Kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye, azirai mahakamani
Kizza Besigye, kiongozi wa upinzani nchini Uganda, amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) katika mji mkuu Kampala baada ya kuanguka na kupoteza fahamu wakati wa kusikilizwa kwa kesi yake ya uhaini.
Besigye, mwenye umri wa miaka 70, amekuwa kizuizini tangu mwezi Novemba 2024.
Wakili wake mkuu alikamatwa mwezi uliopita na kushtakiwa kwa madai ya kushindwa kuripoti vitendo vya uhaini na anazuiliwa na polisi hadi sasa.
Besigye ambaye hali yake ya afya inaonekana kuwa dhaifu, alikuwa akipinga uamuzi wa mawakili wa serikali kuteuliwa kumwakilisha mahakamani, kabla ya kuanguka na kupoteza fahamu. Walinzi wa gereza walimkimbiza hospitalini.
“Bado amepoteza fahamu. Hawezi kuzungumza, na haitikii hata akidungwa sindano ili kupima mwitikio wa maumivu,” mkewe, Winnie Byanyima, ambaye anaongoza shirika la Umoja wa Mataifa linalopambana ugonjwa wa UKIMWI (UNAIDS), amechapisha kwenye mtandao wa X.
Siku ya Jumatano katika Mahakama Kuu ya Kampala, mashahidi waliokuwa mahakamani walisema Besigye alipaza sauti mara kadhaa akisema “wacheni” kuhusu suala la uwakilishi wake wa kisheria kabla ya kuanguka.
Besigye alipelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Mulago, hospitali kubwa zaidi ya umma nchini Uganda, lakini alikataa kutibiwa na wahudumu wa afya wa serikali.
Mkewe Byanyima alisema kupitia X kuwa “Hatutaruhusu afisa yeyote wa serikali kumgusa.”
Mkewe anataka Besigye aruhusiwe kupata matibabu kutoka kwa daktari wake binafsi katika kliniki ya kibinafsi, badala ya kutibiwa katika kituo cha afya cha serikali.
Kitengo cha ICU ambako Besigye anatibiwa, kimezingirwa na maafisa wa usalama . Ripoti zinaeleza kuwa dada yake, ambaye pia ni daktari wake binafsi, ameweza kuruhusiwa kumwona.
Wakili mkuu wa Besigye, Erias Lukwago, yuko gerezani baada ya kukamatwa na jeshi mwezi uliopita.
Wakili wake mwingine Martha Karua kutoka nchini Kenya, alizuiwa kuingia nchini Uganda baada ya kusafiri kwenda huko mwezi uliopita kumwakilisha Besigye.
Mwanawe Besigye, Adam Ampa, amemwomba Rais Yoweri Museveni na mwanawe, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye ni mkuu wa jeshi la Uganda, kuwa na huruma na kumuachilia baba yake kwa misingi ya kibinadamu.
Besigye, ambaye amewania urais dhidi ya Rais Yoweri Museveni mara nne, alitekwa nyara nchini Kenya mwaka wa 2024.
Soma pia: