Wezi wavamia na kuiba vifaa vya mazoezi vya timu ya England

Chanzo cha picha, Getty Images
Timu ya taifa ya England imekumbwa na wizi wa baadhi ya vifaa vyake vya mazoezi kabla ya kuwasili Kansas City siku ya Jumamosi kwa ajili ya Kombe la Dunia 2026.
Chama cha Soka cha England (FA) kinaendelea kufuatilia ni vifaa gani hasa vimeibwa, huku mipira na viatu vya soka vikitajwa kuwa miongoni mwa vitu vinavyohofiwa kutoweka. Tukio hilo lilitokea baada ya magari yaliyokuwa yakisafirisha vifaa kuelekea kituo cha mazoezi cha Swope Soccer Village kuvunjwa.
Kocha Thomas Tuchel na kikosi chake wanatarajiwa kuwasili Kansas City Jumamosi mchana, huku vifaa hivyo vikitarajiwa kuwa tayari kabla ya kuwasili kwao.
Polisi wa Kansas City, wanaoshirikiana na FA katika uchunguzi huo, walifika eneo la tukio Ijumaa usiku. Inaelezwa kuwa watu wawili tayari wamekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Msemaji wa polisi wa Kansas City amesema uchunguzi unaendelea kuhusu uwezekano wa kuibwa kwa vifaa kutoka kwenye gari la timu ambalo liliwasili jijini humo huku baadhi ya vifaa vikitoweka.
Tukio hilo linaweza kuathiri maandalizi ya England kuelekea mchezo wao wa kwanza wa Kombe la Dunia dhidi ya Croatia utakaochezwa Jumatano. Wachezaji wa England wanatarajiwa kufanya mazoezi yao ya kwanza kamili siku ya Jumapili.























