Watu wanaswa katika kituo cha biashara baada ya tetemeko la ardhi kupiga Japan
Chanzo cha picha, Reuters
Watu kadhaa wamenaswa ndani ya kituo cha biashara baada ya tetemeko la ardhi kupiga kusini-magharibi mwa Japan, kulingana na idara ya zimamoto ya eneo hilo.
Mlipuko umeripotiwa kusikika katika kituo cha biashara cha Aeon mjini Kamoto kufuatia atetemeko la ardhi la ukubwa wa 7.1.
Tetemeko hilo lilitokea katika eneo la kisiwa cha Kyushu saa 10:27 jioni kwa saa za ndani (saa 1:27 asubuhi GMT), huku zaidi ya watu 150,000 wakitakiwa kuhamia maeneo salama.
Tahadhari ya tsunami iliyokuwa imetolewa kuwataka wakaazi kuondoka ndani ya saa moja.
Netanyahu kukutana na Trump kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa vita vya Iran
Chanzo cha picha, Getty Images
Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, anatarajiwa kukutakutana na Rais wa Marekani, Donald Trump, katika Ikulu ya White House kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa vita vya siku 40 .
Mkutano huo unafanyika wakati muhimu, huku Trump akisema anafikiria kuanzisha mashambulizi makubwa ikiwa mazungumzo ya Iran yanayoendelea hayatafikia muafaka wowote.
Hii ni mara ya nane kwa Waziri Mkuu wa Israel kukutana na Donald Trump tangu arejee Ikulu ya Marekani (White House), na mkutano huu unafanyika baada ya tofauti kuibuka kati yao kuhusiana na suala la Iran.
Ajenda kuu ya mkutano wa leo kati yaTrump na Netanyahu ni, kwa mara nyingine tena, suala la Iran na vita ambavyo sasa vinakaribia kutimiza miezi sita.
Israel haijashiriki katika awamu ya hivi karibuni ya vita hivyo, lakini katika siku za karibuni imekuwa ikitoa taarifa mara kwa mara kuhusu kudunguliwa kwa ndege zisizo na rubani kwenye mipaka yake.
Netanyahu sio mgeni pekee anayezuru Ikulu ya White House leo.
Rais Volodymyr Zelensky pia yuko Marekani wakati ambapo mvutano kati ya Ukraine na Iran umefikia viwango visivyo na kifani kufuatia shambulio dhidi ya meli ya Iran katika Bahari ya Caspian.
Reuters: Oman yawasilisha kwa Iran pendekezo jipya la kusimamia lango la Hormuz
Chanzo cha picha, Getty Images
Oman imeripotiwa kuwasilisha kwa Iran pendekezo jipya la kuanzisha utaratibu mpya wa kusimamia Mlango-Bahari wa Hormuz, ambao utahusisha ukusanyaji wa ada za hiari kutoka kwa nchi mbalimbali.
Kwa mujibu wa Shirika la habari la Reuters mpango huo unaungwa mkono kikanda.
Chanzo katika eneo hilo, ambacho kiliomba kutotajwa, kiliiambia Reuters kwamba mpango wa Oman unaungwa mkono wa kikanda.
Haya yanajiri baada ya Iran kusema hapo jana kuwa imekataa pendekezo la hapo awali la Oman la kufungua njia ya kusini ya Mlango wa bahari wa Hormuz hadi makubaliano yatakapofikiwa.
Saa chache zilizopita, Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Abbas Araqchi liripoti kuwa amefanya mazungumzo ya simu na wenzao wa Oman na Saudi Arabia.
Saudi Arabia imeyatuhumu makundi ya wanamgambo wa Iraq yanayoshirikiana na Iran kwa kushambulia mitambo yake ya mafuta.
Huku hayo yakijiri Rais Donald Trump amesema kuwa mazungumzo yanaenelea lakini ameonya mazungumzo hayo yasipofikia muafaka wowote, Marekani "itarejelea kufanya kile tulichokuwa tukifanya" kabla ya kusitishwa kwa mashambulizi.
Zidane ateuliwa kuwa kocha wa timu ya taifa ya Ufaransa
Chanzo cha picha, Getty Images
Maelezo ya picha, Zinedine Zidane alishinda Ligi ya Mabingwa mara tatu akiwa kocha wa Real Madrid.
Kocha wa zamani wa klabu ya Real Madrid, Zinedine Zidane, amethibitishwa kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Ufaransa.
Didier Deschamps, kocha aliyedumu kwa muda mrefu zaidi kuinua Ufaransa, alihitimisha kipindi chake cha miaka 14 baada ya timu hiyo kuondolewa katika hatua ya nusu fainali na Uhispania kwenye michuano ya Kombe la Dunia la mwaka 2026.
Zidane, ambaye aliwahi kushinda Kombe la Dunia akiwa na Ufaransa mwaka 1998, hakuwa akihudumia timu yoyote tangu alipoondoka Real Madrid kwa mara ya pili kama kocha mkuu mwaka 2021.
Kocha huyo aliye na umri wa miaka 54, ambaye anachukuliwa na wengi kama mchezaji bora zaidi wa Ufaransa, atasaini mkataba utakaomwezesha kuiongoza timu hiyo katika mchujo wa kufuzu Kombe la Dunia la mwaka 2030.
Baada ya kuteuliwa, alisema ni "fahari kubwa" kuiongoza timu ya taifa ya Ufaransa kufuatia timu hiyo kumaliza katika nafasi ya nne kwenye Kombe la Dunia.
"Nimeshasema mara nyingi: hakuna kitu kikubwa zaidi ya timu ya taifa ya Ufaransa. Hivyo, ni furaha na bila shaka ni fahari kubwa kuwa kocha wa timu hii ya taifa ya Ufaransa," aliongeza.
"Pia ni jukumu. Namshukuru rais wa Shirikisho la Soka la Ufaransa, Philippe Diallo, kamati ya utendaji, na Shirikisho la Soka la Ufaransa kwa imani yao, na kutambua miaka 14 ya utumishi wa Didier na wasaidizi wake."
Diallo alimwelezea kocha mkuu huyo mpya kama "gwiji" wa soka la Ufaransa.
"Uteuzi wa Zinedine Zidane kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Ufaransa ni chanzo cha fahari kubwa kwa Shirikisho la Soka la Ufaransa," alisema.
Maelezo ya picha, Kenya ilipiga marufuku uvutaji shisha tangu mwezi Desemba 2017
Mahakama Kuu imeondoa marufuku ya shisha, ikisema kwamba utekelezaji wake ni kinyume cha sheria na ni kinyume cha katiba.
Akitoa hukumu hiyo Jaji Bahati Mwamuye alisema Sheria za Afya ya Umma (Udhibiti wa Uvutaji wa Shisha) za mwaka 2017 ziliacha kutumika kisheria baada ya serikali kushindwa kuzidhibiti ndani ya kipindi cha miezi tisa kilichotolewa na mahakama mwaka 2018.
Jaji aligundua kuwa mamlaka haikuweza tena kutegemea kanuni zilizokwisha muda wake kutekeleza marufuku, na akatangaza kuwa ni kinyume cha sheria kutolewa kwa vyombo vya habari tarehe 3 Februari 2025 na Aprili 14, 2025 kutangaza kukandamiza maduka ya shisha.
Jaji Mwamuye pia aliamua kuwa kuendelea na utekelezaji wa marufuku hiyo kulikiuka haki za kikatiba za walalamikaji, na kuizuia serikali kutekeleza kanuni hizo zilizokwisha muda wake pamoja na maelekezo yaliyofuata dhidi ya wanachama wa Chama cha Bidhaa Mpya za Tumbaku (Novel Tobacco Products Association).
Haiti kufanya uchaguzi wa kwanza baada ya muongo mmoja
Chanzo cha picha, Reuters
Baraza la uchaguzi la Haiti (CEP) limetangaza Jumatatu kuwa
uchaguzi wa kwanza wa urais baada ya miaka kumi utafanyika mnamo mwezi Desemba,
huku duru ya pili ya uchaguzi ikipangwa kufanyika mwezi Februari.
Awali, uchaguzi huo ulipangwa kufanyika mwezi Agosti na duru
ya pili mwezi Desemba, lakini uliahirishwa kutokana na wasiwasi kuhusu hali ya
usalama.
Haiti haijafanya uchaguzi tangu mwaka 2016.
Rais wake wa mwisho, Jovenel Moise, aliuawa mwaka 2021 baada
ya kuchelewesha kufanyika kwa uchaguzi. Serikali zilizofuata zilipewa jukumu la
kuandaa uchaguzi, lakini zilisema hali ya ukosefu wa usalama kutokana na
mapigano na magenge yenye silaha yenye nguvu imefanya hilo lisiwezekane.
Siku ya Jumatatu, baraza hilo la uchaguzi lilitoa ratiba
inayoonyesha kuwa awamu ya kwanza ya uchaguzi wa rais na wabunge nchini Haiti
itafanyika tarehe 13 Desemba, huku duru ya pili ya uchaguzi ikifanyika tarehe
21 Februari. Pia limetangaza kuwa matokeo ya mwisho yatachapishwa tarehe 7
Machi.
Wananchi pia wanatarajiwa kupiga kura kuhusu mabadiliko ya
katiba pamoja na kuwachagua viongozi wa maeneo ya serikali za mitaa, kulingana
na ratiba hiyo.
Baraza hilo lilisisitiza kuwa utekelezaji wa ratiba hiyo
unategemea "kuwepo kwa hali ya usalama inayokubalika na kupatikana kwa
fedha zinazohitajika kuendesha shughuli za uchaguzi."
Mapema mwezi huu, baraza hilo lilisema limeanza kusajili
wapiga kura na kutoa mafunzo kwa maafisa wa usalama wa uchaguzi. Pia
lilichapisha orodha rasmi ya zaidi ya vyama 300 vya kisiasa vilivyoidhinishwa
kushiriki katika mchakato wa uchaguzi unaokuja.
Chanzo cha picha, Aytac Unal/Anadolu Agency via Getty Images
Chad imekuwa nchi ya hivi karibuni kutangaza mipango ya kujitoa katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) huku nchi hiyo ikidai kwamba kati ya mashauri 13 yaliyochunguzwa tangu mahakama hiyo kuanza kufanya kazi mwaka 2002, tisa yanahusu mataifa ya Afrika.
Chad inajiunga na orodha ya mataifa mengi yanayoituhumu mahakama hiyo ya ICC kwa ubaguzi, huku ikizitaka nchi za Afrika kuimarisha mifumo yao ya sheria ya ndani badala ya kutegemea mahakama za Magharibi.
Kwa mujibu wa serikali ya Chad ni kwamba mahakama hiyo ina ubaguzi dhidi ya mataifa ya Afrika. Burkina Faso, Mali na Niger nazo pia zimeanza mchakato wa kujitoa kutoka Mahakama ya ICC, ambayo inawashtaki watu binafsi kwa makosa ya hatia za kivita na makosa dhidi ya binadamu.
Wakati huo huo, Umoja wa Mataifa umesema uamuzi wa Venezuela kujitoa kutoka Mahakama ya ICC wiki iliyopita unatia wasiwasi mkubwa na utazidisha utamaduni wa kutoadhibiwa kwa ukiukaji wa haki za binadamu. Maafisa wa Venezuela walitangaza kujitoa ICC huku wakidai mahakama hiyo ina ubaguzi wa kijiografia.
Marekani itamaliza fedha za msaada kwa Ukraine Trump atakapoondoka madarakani
Chanzo cha picha, Reuters
Utawala wa Rais wa Marekani Donald Trump umeeleza wajumbe wa
Bunge kwamba hautamaliza kutumia dola milioni 400 ambazo Bunge liliidhinisha
kwa ajili ya msaada kwa Ukraine hadi mwaka wa fedha wa 2029. Haya yanajiri
wakati Ukraine ikikabiliwa na upungufu mkubwa wa silaha muhimu za kujilinda
dhidi ya mashambulizi ya makombora kutoka Urusi.
Mnamo mwezi Mei, Wizara ya Ulinzi ya Marekani iliwatumia
wabunge barua ikieleza mpango wake wa matumizi ya fedha hizo, kwa mujibu wa
chanzo kinachoufahamu waraka huo.
Wanademocrats pamoja na baadhi ya Wabunge wa Chama cha
Republican, ambao pia ni washirika wa Trump, wamekuwa wakiikosoa Wizara ya
Ulinzi kwa kuchelewesha kutoa msaada huo kwa Ukraine, licha ya kwamba
ulipitishwa na wabunge kutoka vyama vyote viwili mwaka uliopita.
Chanzo hicho kilisema kuwa miezi miwili baada ya barua hiyo
kutumwa, fedha hizo bado hazijatolewa wala kutengwa rasmi kupitia mikataba ya
matumizi.
Bunge la Marekani limekuwa likilalamika mara kwa mara juu ya
kasi ya chini ya matumizi ya fedha hizo. Barua hiyo haikuwa imewahi kuzungumziwa
hadharani kabla.
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, anatarajiwa kukutana na
Trump katika Ikulu ya White House siku ya Jumanne, ambapo ataendelea kusisitiza
ombi la Ukraine la kupata mifumo ya ulinzi wa anga inayohitajika kwa haraka,
pamoja na kukamilisha makubaliano ya ushirikiano wa ndege zisizo na rubani
(drones) kati ya Ukraine na Marekani, kwa mujibu wa chanzo kinachofahamu
mipango hiyo.
Baada ya mkutano huo, Zelensky, anatarajiwa kuelekea Bunge
la Marekani (Capitol), ambako atakutana na maseneta wote. Hata hivyo, Baraza la
Wawakilishi liko likizo ya mapumziko ya kiangazi.
Mwimbaji wa Marekani D4vd kujibu tuhuma za mauaji ya msichana (14)
Chanzo cha picha, Getty Images
Jaji wa mahakama moja huko Marekani ameamua kuwa mwanamuziki wa nchini humo, D4vd, atashtakiwa kwa mauaji kuhusiana na kifo cha msichana kijana.
Uamuzi huo ulitolewa baada ya shauri kusikilizwa katika hatua za awali kwa siku tano, ambapo waendesha mashtaka wa Los Angeles waliwahoji mashahidi kadhaa na kuonesha ushahidi wa picha huku familia ya Celeste Rivas Hernandez, mwenye umri wa miaka 14, ikishuhudia.
Nyota huyo, ambaye jina lake halisi ni David Anthony Burke, anatuhumiwa kumuua msichana huyo, ambaye mabaki ya mwili wake yalikutwa Septemba 2025 ndani ya gari aina ya Tesla lililosajiliwa kwa anwani yake.
Burke, mwenye umri wa miaka 21, ameyakana mashtaka ya mauaji na unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya binti huyo.
Kusomewa mashtaka rasmi kwa Burke kumepangwa kufanyika Agosti 31. Kesi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya siku 90 kuanzia tarehe hiyo.
Waendesha mashtaka wanadai kuwa Burke alimchoma kisu msichana huyo na kisha kuukata mwili wake vipande vipande baada ya miaka kadhaa ya madai ya unyanyasaji wa kijinsia.
Wanadai alimuua kwa sababu msichana huyo alitishia kufichua uhusiano wake na mtu aliye chini ya umri wa utu uzima na kuharibu taaluma yake ya muziki yenye thamani ya mamilioni ya dola.
Ushahidi uliowasilishwa mahakamani jana Jumatatu ulionesha vitisho ambavyo Hernandez alimtumia Burke Aprili 22, 2025, kutokana na mabishano kuhusu urafiki wake na msichana mwingine.
"Naapa kwa MUNGU nitakuua," ujumbe mmoja wenye lugha chafu ulisema, ukifuatiwa na tishio la kumnyonga na kumwambia baba yake uongo kumhusu. "Nitaharibu taaluma yako na maisha yako, nitaharibu kila kitu," ujumbe mmoja ulisema.
Siku iliyofuata, Hernandez alikwenda nyumbani kwa Burke huko Hollywood kwa kutumia gari la Uber ambalo Burke alilituma kumchukua. Waendesha mashtaka walidai kuwa Burke alimchoma kisu mara tu alipowasili.
Wakati wa kuhojiwa katika kikao cha mahakama jana Jumatatu, Mpelelezi Corey Farrell wa Idara ya Polisi ya Los Angeles aliiambia mahakama kuwa msichana huyo alikuwa amempa mshtakiwa taarifa zisizo sahihi kuhusu umri wake, kwamba ana umri wa miaka 16 na 18 kwa nyakati tofauti.
Mawakili wa utetezi wa Burke walidai kuwa hakukuwa na ushahidi wa kutosha kuthibitisha kuwa alitenda uhalifu huo.
Twiga Stars yaandika historia kwa kuifunga Afrika Kusini WAFCON 2026
Chanzo cha picha, CECAFA
Tanzania imeandika historia kwa kupata ushindi wake wa kwanza kabisa katika Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) baada ya kuifunga mabingwa wa mwaka 2022, Afrika Kusini, mabao 2 kwa 1 katika mchezo wa ufunguzi wa Kundi B.
Twiga Stars ilitoa moja ya matokeo ya kushangaza zaidi katika mashindano hayo baada ya kuonyesha mchezo wa nidhamu na ujasiri dhidi ya Banyana Banyana, huku Hasnath Ubamba akifunga bao la ushindi dakika ya 87.
Diana Msewa aliitanguliza Tanzania mbele dakika ya 37 baada ya Twiga Stars kuanza mchezo kwa kasi na kulisukuma lango la Afrika Kusini mara kwa mara.
Hata hivyo, Bambanani Mbane aliisawazishia Afrika Kusini katika muda wa nyongeza wa kipindi cha kwanza, na kuifanya timu hizo ziende mapumziko zikiwa sare ya bao 1 kwa 1.
Kipindi cha pili kilikuwa na ushindani mkubwa huku Afrika Kusini ikitafuta bao la ushindi, lakini Twiga Stars iliendelea kujilinda kwa umakini na kutumia mashambulizi ya kushtukiza.
Dakika ya 87, Hasnath Ubamba aliyeingia akitokea benchi aliifungia Tanzania bao la ushindi, lililozua shangwe kubwa miongoni mwa wachezaji, benchi la ufundi na mashabiki.
Ushindi huo ni hatua muhimu kwa soka la wanawake Tanzania. Kabla ya mchezo huo, Twiga Stars ilikuwa imecheza mechi sita za WAFCON bila kushinda, ikipata sare moja na kupoteza tano.
Matokeo hayo pia yanaongeza matumaini ya Tanzania kutinga hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika historia ya mashindano hayo.
Kwa upande wa Afrika Kusini, mabingwa wa mwaka 2022 wameanza vibaya kampeni yao ya kutwaa ubingwa kwa mara nyingine, na sasa watakuwa chini ya shinikizo la kupata matokeo mazuri katika mechi zao zilizosalia za Kundi B ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu hatua inayofuata.
Kwa Twiga Stars, ushindi huo dhidi ya moja ya timu zenye nguvu zaidi barani Afrika unaweza kuwa chachu ya kujiamini katika harakati za kuandika historia nyingine kwenye WAFCON 2026.
Wakati huo huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Timu ya Taifa ya Wanawake ya Tanzania, Twiga Stars, kwa kuanza vyema michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026 nchini Morocco.
“Ninaungana na Watanzania wote kuitakia kila la kheri Twiga Stars inapoendelea kupeperusha bendera ya Taifa letu katika michezo inayofuata. Endeleeni kupambana kwa moyo huo huo, mkionyesha uzalendo, nidhamu na ari ya ushindani inayolitangaza vyema Taifa letu,” amesema Rais Samia Suluhu Hassan.
Dunia iko katika hatari ya kuongezeka kwa maambukizi ya VVU - UNAIDS
Chanzo cha picha, AFP via Getty Images
Shirika la
Umoja wa Mataifa linalopambana na UKIMWI limesema dunia iko katika hatari ya
kushuhudia kuongezeka tena kwa janga la maambukizi ya VVU baada ya ufadhili wa
kimataifa kupunguzwa kwa karibu asilimia 20 mwaka uliopita.
Katika
ripoti iliyotolewa kuadhimisha ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa UKIMWI
nchini Brazil, UNAIDS ilisema ufadhili ulipungua hadi takriban dola bilioni
saba za Marekani, kiwango cha chini zaidi katika karibu miongo miwili.
"Ni
ripoti inayoonyesha mambo mawili, kwanza ni kuhusu maendeleo ya kisayansi na
pili ni onyo kwamba kuondolewa kwa misaada inaleta kukosekana kwa usawa kunakoathiri
haki za binadamu. Na kuweka maisha katika miongo kadhaa hatarini," amesema
Winifred Byanyima, Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS.
Byanyima ameongeza
kuwa kwa sasa matwakwa ya kisiasa ndio yanayoamua namna ya kupambana na virusi
vya UKIMWI na si masuala ya kisayansi
"Swali
sio tena kama tunaweza kumaliza UKIMWI, bali ni je, tunachagua kumaliza Ukimwi.
Harakati za kupambana na ukimwi kwa sasa hazikumbwi na changamoto za kisayansi
bali zinakabiliwa na kukosekana kwa usawa kutokana na msukumo wa kisiasa. Kama
tunatokomeza ukimwi haitaamuliwa maabara, basi ni matwaka ya kisiasa,"
amesema Byanyima.
Marekani ilikuwa
ikichangia takriban robo tatu ya ufadhili wa kimataifa wa mapambano dhidi ya
VVU kabla ya Rais Trump kurejea madarakani mnamo Januari 2025.
Moto wa nyika: Macron asema Ufaransa inakabiliwa na hali mbaya zaidi tangu Vita vya Pili vya Dunia
Chanzo cha picha, EPA/Shutterstock
Rais wa
Ufaransa, Emmanuel Macron, ameahidi kutumia kila rasilimali iliyopo kupambana
na moto mkubwa wa nyika unaoendelea nchini humo akisema janga hilo ni mbaya
zaidi kuwahi kuikumba Ufaransa tangu Vita vya Pili vya Dunia.
Rais wa
Ufaransa, Emmanuel Macron, ameonya kuwa hali itaendelea kuwa ngumu zaidi
alipokuwa akitembelea kituo cha operesheni za kuzima moto katika eneo la
Gironde, ambalo limeathiriwa vibaya na moto huo uliosababisha mioto mikubwa
isiyoweza kudhibitiwa.
Akizungumza
na vikosi vya zimamoto na wahudumu wa dharura, Macron alisema:
"Tunakabiliwa
na hali ngumu zaidi kuwahi kushuhudiwa, hali ambayo haijawahi kutokea tangu
Vita vya Pili vya Dunia."
Aliongeza
kuwa msimu wa moto wa nyika, ambao kwa kawaida hufikia kilele mwezi Agosti,
bado haujaanza kikamilifu.
Rais Macron
ameonya kuwa viwango vya joto vinatarajiwa kupanda tena, akisisitiza kuwa cha
msingi kwa sasa ni kuokoa maisha.
Wakati huo
huo, wazima moto nchini Uhispania wamekuwa wakipambana kudhibiti baadhi ya moto
mbaya zaidi wa nyika katika historia ya hivi karibuni ya nchi hiyo huku kukiwa
na onyo la wimbi kubwa la joto linaloongezeka ambalo linaweza kuzorotesha zaidi
hali hiyo.
Viwango vya
joto katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo vinatarajiwa kuwa ya juu zaidi.
Waziri Mkuu,
Pedro Sanchez, ameonya kuwa ni wakati mgumu kwa nchi yake huku akitoa wito kwa
vyama vya kisiasa kuweka kipaumbele katika kuunda mkataba wa kitaifa wa dharura
wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Johnson & Johnson yajitolea kulipa hadi $5.5bn kumaliza kesi za poda ya watoto
Chanzo cha picha, Getty Images
Kampuni ya
Johnson & Johnson (J&J) imejitolea kulipa hadi dola bilioni 5.5 (pauni
bilioni 4.14) ili kumaliza maelfu ya kesi zinazodai poda yake ya watoto pamoja
na bidhaa nyingine zenye madini ya talcum husababisha saratani ya ovari au kifuko
cha mayai.
Makubaliano
hayo makubwa yanakusudia kumaliza mzozo wa kisheria uliodumu kwa miaka kadhaa
na kuendelea kuigharimu kampuni hiyo kubwa ya huduma za afya nchini Marekani.
J&J
imeendelea kusisitiza kuwa bidhaa zake zenye talcum hazisababishi saratani, na
tayari imebadilisha viambato vya poda yake ya watoto inayotumiwa na watu wengi.
Makamu wa
Rais wa masuala ya kesi za kisheria wa kampuni hiyo, Erik Haas, alisema
Jumatatu kuwa madai hayo "hayana msingi", na kwamba J&J imeamua
kufikia makubaliano ili kutatua kabisa suala hilo.
Kampuni hiyo
imesema makubaliano hayo yatahusisha takriban kesi 69,000, ambazo ni sehemu
kubwa ya madai yaliyosalia yanayohusiana na bidhaa za talcum. J&J imeeleza
kuwa italipa hadi dola bilioni 3 mwaka ujao, na kusitarajiwe malipo mengine kabla
ya mwaka 2028.
J&J pia
imesema pendekezo hilo litalazimika kukubaliwa na kampuni za mawakili
zinazowawakilisha asilimia 95 ya walalamishi wa kesi za saratani ya ovari
katika mahakama za majimbo na za shirikisho, kabla ya makubaliano hayo
kukamilika.
Katika
taarifa yake, Haas alisema kampuni ina imani kuwa ingeibuka mshindi endapo kesi
hizo zingeendelea mahakamani, kama ilivyofanikiwa katika kesi nyingi ambazo
tayari zimeamuliwa.
Aliongeza
kuwa makubaliano hayo yataiwezesha kampuni kuhitimisha suala hilo na kuelekeza
nguvu zake katika jukumu lake la kutengeneza dawa na vifaa vya tiba vinavyookoa
maisha.
Mazungumzo ya vita vya Iran yanaendelea huku mashambulizi yakisitishwa - Trump
Chanzo cha picha, Reuters
Rais wa
Marekani, Donald Trump, amesema kuwa kuna "mazungumzo ya kirafiki yanayoendelea"
kuhusu mzozo wa Iran, baada ya pande zinazopigana kutoshambuliana kwa siku ya
tatu mfululizo.
Akiwa ndani
ya ndege ya Air Force One siku ya Jumatatu, Trump alieleza matumaini yake
kwamba vita hivyo vinaweza kufikia mwisho. Aliwaambia waandishi wa habari: "Ninaamini
kuna uwezekano mkubwa jambo fulani likatokea."
Alionyesha
matumaini kwamba vita vinaweza kumalizika Jumatatu, akiwaambia waandishi wa
habari ndani ya ndege ya Air Force One: "Nafikiri kuna fursa nzuri ya
kutokea kwa jambo fulani."
Hata hivyo,
alionya kuwa iwapo mazungumzo hayo hayatakuwa na mafanikio, Washington
"itarejea kufanya kile tulichokuwa tukifanya" kabla ya kusitishwa kwa
mashambulizi.
Kwa upande
wake, Tehran imekanusha kuwa kuna mazungumzo yoyote ya moja kwa moja
yanayoendelea.
Trump
alisema aliamua kusitisha mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran siku ya Ijumaa
baada ya nchi zinazosaidia kupatanisha pande hizo kumwomba kutoa fursa nyingine
kwa mazungumzo.
Iran pia
imesitisha mashambulizi yake.
Hatua hiyo inafuatia
karibu wiki mbili za mashambulizi ya kila siku ya Marekani na ya kulipizana
kisasi kati ya pande hizo, hali iliyovuruga kwa kiasi kikubwa makubaliano ya
usitishaji mapigano yaliyofikiwa mnamo mwezi Juni.
Wakati huo,
jeshi la Marekani lilisema mashambulizi yake yalilenga kupunguza uwezo wa Iran
wa kuhatarisha usafirishaji wa meli za kibiashara katika Mlango Bahari wa
Hormuz, ambao ni njia muhimu duniani ya usafirishaji wa mafuta.