Moja kwa moja, Meli ya abiria yaungua moto, watu 5 wafariki na zaidi ya 87 hawajulikani walipo

Meli hiyo, MV June Aster, ilikuwa imebeba watu 134, wakiwemo abiria 117 na wafanyakazi 17. Mamlaka zinasema watu 42 wameokolewa na shughuli za utafutaji na uokoaji zinaendelea.

Moja kwa moja

Na Yusuph Mazimu

  1. Kila Mmarekani atapata dola 5,000 Republican ikishinda uchaguzi wa katikati ya muhula - Trump

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema atampa kila Mmarekani mtu mzima dola 5,000 iwapo chama cha Republican kitashinda mihula yote miwili ya Congress katika uchaguzi wa katikati ya muhula utakaofanyika Novemba — mpango ambao unaweza kugharimu zaidi ya dola trilioni moja.

    Ahadi hiyo ilitolewa katika hotuba yake kwenye mkutano wa kwanza kabisa wa chama hicho kufanyika katikati ya muhula wa urais nchini Marekani.

    Trump hakutoa maelezo kuhusu mpango huo utakavyotekelezwa au utakavyofadhiliwa, akisema tu kuwa fedha hizo zitatakiwa kutumika nchini Marekani. Makamu wa Rais JD Vance ameihusisha mipango hiyo na mapato ambayo serikali ya Marekani imekusanya kupitia ushuru wa bidhaa unaotozwa na Trump.

    Mpango huo umezua utata. Wademokrasia wameuita “ahadi tupu”, huku wengine wakihoji iwapo ahadi kama hiyo inaruhusiwa kisheria.

    Huenda hii ikawa mara ya kwanza kwa rais wa Marekani kutoa ahadi ya malipo ya aina hiyo kwa Wamarekani, katika mazingira ya mwaka wa uchaguzi ambapo anawahimiza wananchi kujitokeza na kupiga kura.

    Iwapo mpango huo unawezekana au la, haikuonekana kuwa jambo la msingi kwa wakati huo. Wazo hilo lilipokelewa kwa makofi na shangwe kubwa kwenye mkutano huo, huku Trump akionekana kufurahia mwitikio huo.

    Kuna karibu Wamarekani watu wazima milioni 270, hivyo malipo ya dola 5,000 kwa kila mtu yangegharimu serikali ya Marekani takriban dola trilioni 1.3.

    Maswali yameanza kuibuka kuhusu uwezekano wa kutekelezwa kwa mpango huo, hasa wakati bei za bidhaa nchini Marekani zikiendelea kupanda, kwa kiasi fulani kutokana na vita ya Marekani na Israel dhidi ya Iran ilioanza mwezi Februari.

    Mashambulizi ya kulipiza kisasi ya Iran yamejumuisha kushambulia kambi za kijeshi za Marekani na washirika wake katika Ghuba. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba Iran kwa kiasi kikubwa imefunga Mlango-Bahari wa Hormuz, ambao hupitisha takriban theluthi moja ya biashara ya mafuta duniani pamoja na sehemu kubwa ya gesi asilia iliyoyeyushwa.

    Kufungwa kwa njia hiyo kumesababisha mabadiliko makubwa ya bei ya mafuta duniani, huku Trump akikabiliwa na shinikizo kutoka ndani ya chama chake kumaliza vita hivyo.

    Jumatano, rais huyo wa Marekani aliwaonya wafuasi wake kwamba vita hivyo havitamalizika hadi baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula, na kwamba bei ya mafuta haitashuka hadi wakati huo.

    Alitoa kauli hiyo kabla ya hotuba yake huko Texas, na kuirudia katika mkutano wa chama chake, ambapo alisisitiza kuwa maumivu ya kiuchumi ya muda mfupi yanafaa kuvumiliwa ili kuzuia Tehran kutengeneza silaha za nyuklia.

    Unaweza kusoma;

  2. Rodri aomba radhi kwa kauli kuhusu Valencia kuwa 'dhaifu'

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kiungo wa Barcelona, Rodri, amesema ameiomba radhi timu nzima ya Valencia baada ya kamera za televisheni kuonekana kumnasa akisema kuwa klabu hiyo inayosuasua kwenye La Liga ni “dhaifu sana.”

    Rodri anadaiwa kutoa kauli hiyo akiwa amekaa kwenye benchi baada ya kutolewa uwanjani katika ushindi wa Barcelona wa mabao 5-0 dhidi ya Valencia katika mchezo wa ligi Jumapili.

    Matokeo hayo katika Uwanja wa Mestalla yaliiacha Valencia mkiani mwa msimamo wa ligi, ikiwa haijapata ushindi wowote katika michezo yake minne ya kwanza.

    Ingawa video hiyo haina sauti, kituo cha televisheni cha Movistar kilidai kuwa kilisoma mwendo wa midomo ya Rodri, mwenye umri wa miaka 30 na aliyewahi kuichezea Manchester City, na kubaini akisema:

    “Wao ni dhaifu sana. Hawajavuka hata mstari wa nusu ya uwanja.”

    Mashabiki pamoja na baadhi ya vyombo vya habari nchini Hispania walimshutumu Rodri kwa kukosa heshima.

    Rodri, ambaye alishinda tuzo ya Golden Ball baada ya Uhispania kutwaa Kombe la Dunia la 2026, alisema baada ya Barcelona kuifunga Feyenoord 5-1 katika Ligi ya Mabingwa Jumatano:

    “Niliomba radhi kwa rafiki na mwenzangu Jose Gaya [nahodha wa Valencia na beki wa Uhispania], pamoja na kikosi kizima.”

    “Pia ninataka kuweka wazi kwamba ilikuwa tu kauli ya mshangao. Mtu yeyote anayeitazama video hiyo anaweza kuona hilo.”

    “Kwa vyovyote vile, sikukusudia kumdhihaki mtu yeyote wala kutumia vibaya hali ngumu ambayo timu hiyo inapitia. Kinyume chake, sote tunataka Valencia irudi katika nafasi inayostahili kwenye ligi. Ni moja ya klabu bora katika mashindano haya. Hilo ndilo nililotaka kusema.”

    “Pia ningependa kuongeza kwamba hayo yalikuwa mazungumzo ya faragha. Nafikiri sote tunapaswa kujifunza zaidi kutokana na hili, kwa sababu wakati mwingine mambo huweza kutolewa kwenye muktadha wake.”

    “Lakini kwa vyovyote vile, sikukusudia kumkosea mtu yeyote heshima. Naomba radhi kwa Valencia.”

    Unaweza kusoma;

  3. Iran yataka UN kuingilia vikwazo vya anga vya Marekani dhidi yake

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Iran imeutaka Umoja wa Mataifa kuingilia kati uamuzi wa Marekani wa kuweka vikwazo vipya dhidi ya sekta yake ya usafiri wa anga, ikionya kuwa hatua hiyo inaweza kuwa na athari kubwa kwa raia wa kawaida.

    Katika barua iliyowasilishwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Tehran ilivitaja vikwazo dhidi ya mashirika 27 ya ndege ya Iran na taasisi zinazohusiana na sekta hiyo kuwa "ugaidi wa kiuchumi, adhabu ya pamoja na uhalifu dhidi ya binadamu."

    Iran inasisitiza kuwa hatua hiyo ni ukiukaji wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa na sheria za kimataifa zinazolenga kulinda raia, ikidai kuwa vikwazo hivyo vinaweza kuathiri shughuli za kawaida za usafiri wa anga na huduma muhimu zinazotegemea sekta hiyo.

    Katika malalamiko yake, Iran imeliomba Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pamoja na Katibu Mkuu wa Umoja huo kuzitaka nchi wanachama kutozitambua wala kutekeleza hatua hizo za Marekani.

    Hatua hiyo ya Tehran imekuja siku chache baada ya Washington kutangaza kupanua wigo wa vikwazo vyake kwa kuongeza mashirika yote ya ndege ya Iran ambayo hayakuwa tayari yameorodheshwa kwenye orodha ya vikwazo vya kiuchumi.

    Vikwazo hivyo havihusu tu mashirika ya ndege ya Iran, bali pia kampuni kadhaa zinazofanya kazi katika sekta ya anga zenye makao katika Falme za Kiarabu, Uturuki, Malaysia na Kazakhstan.

    Afisa mmoja wa Wizara ya Fedha ya Marekani, aliyenukuliwa na shirika la habari la AFP bila kutajwa jina, alisema lengo la hatua hiyo ni kuiondoa sekta ya usafiri wa anga ya Iran kutoka katika soko la kimataifa.

    Miongoni mwa mashirika yaliyoathirika ni Iran Air, Shirika la Taifa la Ndege la Iran, ambalo liliondolewa kwenye vikwazo chini ya makubaliano ya nyuklia ya mwaka 2015 (JCPOA) kabla ya kurejeshwa tena baada ya Marekani kujiondoa kwenye makubaliano hayo mwaka 2018.

    Mvutano huo ni sehemu ya mgogoro wa muda mrefu kati ya Tehran na Washington kuhusu matumizi ya vikwazo vya kiuchumi, ambapo Iran imekuwa ikishutumu Marekani kwa kutumia adhabu za kiuchumi kama nyenzo ya shinikizo la kisiasa dhidi yake.

    Soma pia:

  4. Uteuzi wa mwanahabari kuwa mfalme baada ya kifo cha Oyo wazua mzozo Uganda

    .

    Chanzo cha picha, AP

    Maelezo ya picha, Mflame Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV, enzi za uhai wake akisheherekea kutimiza miaka 18 tarehe 17 April 2010

    Mzozo wa urithi katika Ufalme wa Tooro nchini Uganda umeshika kasi siku chache kabla ya mazishi ya marehemu Mfalme Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV, huku familia ya kifalme ikipinga uteuzi wa Mwanamfalme Edward Rukidi Kijanangoma kuwa mrithi wake.

    Mwanamfalme Kijanangoma, ambaye ni binamu wa marehemu Mfalme Oyo, ni mtangazaji wa habari na mhariri katika shirika la utangazaji la taifa la Uganda, UBC. Ukoo wa kifalme wa Tooro ulimteua siku ya Jumatano baada ya mchakato wa kutafuta mrithi.

    Anatarajiwa kutawazwa wiki hii, kabla ya mazishi ya Mfalme Oyo yanayotarajiwa kufanyika Jumamosi na kuhudhuriwa na makumi ya maelfu ya waombolezaji. Mfalme Oyo alifariki mwezi uliopita akiwa na umri wa miaka 34 baada ya kuugua saratani, na hakuwa ameoa.

    Mama wa marehemu mfalme, Malkia Best Kemigisa, amesema walinzi wa kifalme wameondolewa katika Makazi yake (Ikulu) ambayo imezungukwa na wanajeshi wa jeshi la Uganda. Amesema hali hiyo imeizuia familia ya kifalme kutoka na kupokea wageni, akielezea hali hiyo kama “kizuizi cha nyumbani”.

    Dada yake Mfalme Oyo, Ruth Komuntale, amesema familia “imekatishwa tamaa” na uamuzi wa kumteua Kijanangoma na kwamba wosia wa marehemu ulieleza wazi kuwa aliacha mrithi wa kiti cha ufalme.

    Awali Rais wa Uganda Yoweri Museveni alisema Mfalme Oyo aliacha mtoto wa kiume ambaye angeweza kuwa mrithi, ingawa inadaiwa alizaliwa nje ya ndoa. Hata hivyo, kamati ya Tooro ilimchagua Mwanamfalme Kijanangoma.

    Ufalme wa Tooro ni miongoni mwa falme tano za jadi zinazotambuliwa na serikali ya Uganda, ingawa hazina mamlaka rasmi ya kisiasa. Falme hizo zilipigwa marufuku baada ya Uganda kupata uhuru, kabla ya kurejeshwa mwaka 1993.

    Mfalme Oyo alitawazwa mwaka 1995 akiwa na umri wa miaka mitatu baada ya kifo cha baba yake. Alikuwa akijulikana kama “mfalme mtoto” na aliongoza ufalme huo kwa msaada wa wasimamizi hadi alipofikisha umri wa miaka 18.

  5. Meli ya abiria yaungua moto, watu 5 wafariki na zaidi ya 87 hawajulikani walipo

    .

    Chanzo cha picha, Philippine Coast Guard

    Watu watano wamefariki na wengine 87 hawajulikani walipo baada ya meli ya abiria kushika moto katika bahari karibu na Palawan, Ufilipino, Jumatano.

    Mamlaka za nchi hiyo zinasema watu 42 wameokolewa na shughuli za utafutaji na uokoaji zinaendelea.

    Meli hiyo, MV June Aster, ilikuwa imebeba watu 134, wakiwemo abiria 117 na wafanyakazi 17. Ilikuwa ikisafiri kutoka Manila kuelekea Coron, Palawan, iliposhika moto katika eneo lililokuwa karibu kilomita 2.2 kutoka kaskazini-mashariki mwa Barangay Marcilla.

    Inaelezwa kuwa idadi ya watu ambao hawajulikani walipo ni 87 kwa mujibu wa taarifa za sasa, lakini idadi hiyo inaweza kubadilika wakati shughuli za utafutaji zikiendelea. Kati ya waliookolewa, 38 ni abiria na wanne ni wafanyakazi wa meli.

  6. Arsenal haikamatiki, Liverpool yang'ara Madrid katika Ligi ya Mabingwa

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Arsenal imeanza kampeni yake ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa ushindi wa 1-0 ugenini dhidi ya Napoli, huku nahodha Martin Odegaard akiendelea kuonyesha kiwango bora baada ya kufunga bao pekee la mchezo. Liverpool nayo imeanza vyema kwa kuichapa Atletico Madrid 2-1, huku Barcelona ikiifunga Feyenoord 5-1.

    Paris Saint-Germain imepata ushindi mkubwa zaidi wa usiku huo baada ya kuifunga Slovan Bratislava 6-1. Sporting CP pia imeanza kampeni kwa ushindi wa 3-1 dhidi ya Galatasaray, wakati Stuttgart imeifunga Viking 3-1.

    Ushindi wa Arsenal dhidi ya Napoli ulitokana na bao la Odegaard dakika ya 75, akipiga shuti kali kwa mguu wa kushoto lililomshinda kipa Jan Oblak. Arsenal ilitawala mchezo huo kwa sehemu kubwa na kuondoka na alama zote tatu.

    Kwa upande wa Liverpool, Alexis Mac Allister alifunga bao la ushindi dhidi ya Atletico Madrid, siku moja baada ya kuzungumza kwa hisia kuhusu kutopatiwa mkataba mpya na klabu hiyo. Mchezaji huyo wa Argentina alionyesha thamani yake uwanjani kwa kuisaidia Liverpool kupata ushindi huo wa 2-1.

    Matokeo hayo yanaifanya Arsenal, Liverpool, Barcelona na PSG kuanza hatua ya ligi kwa ushindi, huku Arsenal ikitoa ishara nyingine ya uwezo wake wa kushindania tena mataji makubwa msimu huu.

  7. Iran yashambulia kituo cha Marekani Jordan na kuharibu ndege za kijeshi

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    CBS News imeripoti, ikinukuu vyanzo vyenye ufahamu wa moja kwa moja kuhusu tukio hilo, kwamba ndege kadhaa za kijeshi za Marekani ziliharibiwa katika shambulio la makombora ya Iran dhidi ya kituo cha anga cha Mowaffaq Salti nchini Jordan mapema Jumatano asubuhi, kwa saa za huko.

    Vyanzo hivyo, vilivyozungumza bila kutajwa majina kutokana na unyeti wa suala hilo, vilisema takriban ndege nane za kivita aina ya F-15 zilipata uharibifu mdogo, lakini zilirudi katika operesheni baada ya kutengenezwa.

    Vyanzo hivyo pia vilisema ndege ya mashambulizi aina ya A-10 Thunderbolt, inayojulikana kama “Warthog”, ilipoteza moja ya mabawa yake baada ya kugongwa na kombora.

    Kwa mujibu wa CBS, chanzo cha ujasusi kinachofahamu suala hilo kiliwaambia kwamba hakuna mwanajeshi wa Marekani aliyeuawa katika mashambulizi hayo.

    Mashambulizi hayo yalitokea saa kadhaa baada ya Marekani kusema imezishambulia meli tano za mafuta za Iran, ikisema hatua hiyo ilikuwa ya kujibu shambulio la Iran dhidi ya meli ya kivita ya Jeshi la Wanamaji la Marekani.

    Walinzi wa Mapinduzi ya Iran pia walisema walilenga meli nane za mafuta na meli mbili za kivita za Marekani, pamoja na kituo cha anga cha Mowaffaq Salti nchini Jordan.

    CBS pia iliripoti kwamba majeshi ya Marekani nchini Jordan yalifyatua makombora zaidi ya 30 ya Patriot kuzuia mashambulizi hayo.

  8. Tetesi za Soka Ulaya: Man Utd na Spurs zinamfuatilia Tresoldi

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Manchester United na Tottenham zote zilikuwa na wawakilishi nchini Ubelgiji Jumanne kumtazama mshambuliaji wa Ujerumani Nicolo Tresoldi, 22, wa Club Brugge. (Teamtalk, external)

    Newcastle bado inaweza kumuuza Lewis Hall majira ya joto yajayo licha ya beki huyo wa kushoto wa England mwenye umri wa miaka 22, ambaye hivi karibuni alihusishwa na uhamisho kwenda Manchester United, kuripotiwa kukubaliana mkataba mpya na Magpies hadi 2031. (Talksport, external)

    Lisandro Martinez, 28, atapewa mkataba mpya wa muda mrefu na Manchester United iwapo beki huyo wa kati wa Argentina ataendelea kuwa fiti bila majeraha na kufanya vizuri katika msimu wa 2026-27 huko Old Trafford. (Football Insider, external)

    Brighton wana imani kuwa mkataba mpya wa kiungo wa Sweden Yasin Ayari, 22, unaweza kukubaliwa hivi karibuni huku mazungumzo yakiendelea vizuri. (Teamtalk, external)

    Hata hivyo, mustakabali wa Kaoru Mitoma huko Brighton bado haujulikani, huku winga huyo wa Japan mwenye umri wa miaka 29 akitarajiwa kutoongeza mkataba wake unaomalizika majira ya joto yajayo na anaweza kuondoka mapema katika dirisha la Januari. (Teamtalk, external)

    Baada ya kushindwa kumsajili kiungo wa Ufaransa Manu Kone majira ya joto, Chelsea inaweza kurejea kumsajili mchezaji huyo wa AS Roma, mwenye umri wa miaka 25, mwezi Januari katika dili ambalo pia linaweza kumhusisha winga wa England Jamie Gittens, 22, kuelekea upande mwingine. (Simon Phillips, via CaughtOffside, external)

    Liverpool wana mipango ya kumsajili kiungo mwingine majira ya joto yajayo, jambo ambalo litamshusha zaidi Alexis Mac Allister, 27, kwenye kupata namba katika kikosi huko Anfield. (Talksport, external)

    Atletico Madrid hawana mpango wa kumuuza kiungo wa Hispania, Alex Baena, 25, hivi karibuni licha ya Manchester City kuvutiwa naye (Football Insider, external)

    Beki wa Austria David Alaba anaweza anaswaka na klabu ya Mexico Club Amerika baada ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 34 kuondoka Real Madrid majira ya joto. (Fichajes - in Spanish, external)

  9. Trump: Vita vya Iran vinaweza kumalizika baada ya uchaguzi wa Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema haamini kuwa vita vya Iran vitaisha kabla ya uchaguzi wa katikati ya muhula wa Marekani wa Novemba, akiongeza kuwa bei ya mafuta pia haitashuka hadi wakati huo.

    “Nadhani vita vitaisha mara tu baada ya uchaguzi kwa sababu hawawezi kuendelea tena,” Trump alisema Jumatano, akizungumzia Iran.

    Kauli hiyo aliitoa akiwa njiani kuelekea Texas kuhudhuria mkutano wa kwanza wa chama chake wa kuelekea uchaguzi huo wa katikati ya muhula, ambao unaweza kubadilisha nguvu ndani ya serikali ya Marekani.

    Trump anakabiliwa na kushuka kwa umaarufu katika kura za maoni, pamoja na shinikizo kutoka ndani ya chama chake cha Republican la kutaka amalize vita na Iran.

    Jumatano, bei ya mafuta ilipanda hadi dola 100 (£74) kwa pipa kwa mara ya kwanza tangu Julai, kutokana na kuongezeka kwa mapigano Mashariki ya Kati.

    “Mara tu baada ya uchaguzi, bei ya mafuta itaporomoka,” Trump aliwaambia waandishi wa habari. “Nadhani itachukua muda mrefu kidogo kuliko uchaguzi wa katikati ya muhula.”

    Aliongeza kuwa Iran ilikuwa “imekata tamaa kujaribu kuathiri uchaguzi, ili tupate kundi la watu dhaifu” akionekana kumaanisha chama cha Democrats “na kuwaacha peke yao na kuruhusu wapate silaha zao za nyuklia”.

    Tehran imekanusha mara kwa mara kuwa inatafuta kutengeneza silaha za nyuklia.

  10. Habari na karibu katika taarifa zetu za moja kwa moja leo