Takriban Warundi 600 wazuiliwa mpakani Kenya na Tanzania

Chanzo cha picha, Getty Images
Takriban Warundi 600 wanaorejea nchini Burundi kutoka Kenya wamezuiliwa katika mpaka wa Isebania, kwa sababu hawana hati za kusafiria.
Mkuu wa chama cha Waburundi wanaoishi Kenya, Alexis Ntinanirwa, ameiambia BBC Gahuzamiryango kuwa watu hao walikuwa kwenye magari mbalimbali, lakini maafisa wa uhamiaji waliwazuia kuvuka mpaka katika upande wa Sirari, Tanzania.
Amesema Ubalozi wa Burundi nchini Kenya unafahamu hali hiyo na unaendesha mazungumzo na serikali za Kenya na Tanzania, ili kuruhusu Warundi hao kuendelea na safari bila kulazimika kurejea Nairobi kuchukua hati za kusafiria.
Kwa sasa, amesema, wako katika uwanja wa mpira mpakani wakisubiri uamuzi.
Bw. Ntinanirwa amesema shirika lao, kwa kushirikiana na Ubalozi wa Burundi nchini Kenya, pia linafanya mazungumzo na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM), Shirika la Msalaba Mwekundu na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), ili kuwapatia msaada wa haraka, ukiwemo chakula na malazi.
Ameongeza kuwa upatikanaji wa magari ya kuwasafirisha Warundi wanaotaka kurejea nchini humo ni changamoto nyingine inayoshughulikiwa.
Hali hiyo inajiri huku mamia ya Warundi wakiwa wamekuwa wakikusanyika kwa siku kadhaa katika Ubalozi wa Burundi jijini Nairobi, wakitafuta hati za kusafiria ili kurejea nyumbani.
Wanasema wanahofia matamshi ya Rais wa Kenya, William Ruto, kuhusu wafanyabiashara wadogo wa kigeni.
Serikali ya Kenya imewapa raia wa kigeni siku 90 kukamilisha taratibu zinazohitajika ili kuishi, kufanya kazi na biashara nchini humo. Pia imesema hakuna mtu au kundi linaloruhusiwa kuwatisha, kuwanyanyasa au kuwazuia wageni kuendelea na shughuli zao.
Hata hivyo, baadhi ya Warundi wameiambia BBC kuwa bado wanataka kurejea nyumbani kwa sababu hawaamini kuwa watalindwa.
Ingawa Burundi, Kenya na Tanzania ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, wasafiri wanaovuka mipaka wanatakiwa kuwasilisha pasipoti au hati nyingine halali ya kusafiria.
Pia unaweza kusoma:


