Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran na Marekani zashambuliana tena, utulivu wa muda mfupi wasambaratika

Tukio hilo limekatiza kipindi kifupi cha utulivu kilichokuwa kimeanza kurejesha matumaini ya mazungumzo kati ya pande hizo mbili.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Ghana yaomboleza kifo cha mwanaume mrefu zaidi nchini humo

    Kifo cha Sulemana Abdul Samed, aliyekuwa mwanaume mrefu zaidi nchini Ghana, kimezua majonzi makubwa, hasa kaskazini mwa nchi ambako urefu wake ulimfanya kuwa mtu maarufu katika jamii.

    Sulemana mwenye umri wa miaka 33 alifariki dunia akiwa hospitalini Jumatatu katika mji wa Tamale, ulioko takriban kilomita 160 kusini mwa kijiji chake cha Gambaga alikokuwa amelazwa baada ya vidonda vya miguu yake kupata maambukizi.

    "Kila mtu alijua jinsi alivyokuwa mkarimu na mwenye moyo mwema. Tangu alipofariki hadi sasa, watu wengi bado wanaendelea kufika nyumbani kujua kilichotokea," amesema ndugu yake, Sulemana Abdul Kudus, alipozungumza na BBC.

    Sulemana aligundulika kuwa na ugonjwa nadra unaosababisha watoto kukua kupita kiasi na kufikia urefu usio wa kawaida akiwa katika miaka yake ya ishirini.

  2. Uamuzi wa mahakama ya DRC wamfungulia njia ya muhula wa tatu Tshisekedi

    Uamuzi wa mahakama ya DRC wamfungulia njia ya muhula wa tatu Tshisekedi

    Mahakama ya Kikatiba ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo imeidhinisha sheria muhimu ya kura ya maoni, hatua ambayo huenda ikamfungulia Rais Félix Tshisekedi njia ya kugombea muhula wa tatu madarakani.

    Mwenyekiti wa Mahakama hiyo amesema muswada huo, uliopitishwa na Bunge la Seneti mnao mwezi Juni, unaendana na Katiba, hivyo kuidhinisha vifungu vinavyoruhusu kufanyiwa marekebisho.

    Upinzani umelaani sheria hiyo, ukisema suala hilo linarejesha nyuma juhudi za kutatua mzozo wa muda mrefu unaoendelea mashariki mwa Congo.

    Maelfu ya watu wameandamana katika miji ya mashariki wa Goma na Bukavu kupinga hatua hiyo.

    Rais Tshisekedi amebakisha miaka miwili katika muhula wake wa pili na wa mwisho wa uongozini.

  3. Zelensky, Netanyahu wakutana na Trump huku vita vya Ukraine na Iran vikiendelea

    Rais Donald Trump amefanya mikutano tofauti na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky pamoja na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, mikutano ambayo Ikulu ya Marekani ilielezea kuwa ya "kujenga na yenye tija".

    Viongozi hao wawili walikuwa Washington kuhudhuria maziko ya Seneta Lindsey Graham, ambaye alikuwa mfuasi mkubwa wa Israel na mtetezi wa misaada ya Marekani kwa Ukraine, ambaye alifariki dunia mapema mwezi huu.

    Zelensky na Trump walijadili matumaini ya Kyiv kwamba Marekani ingesaidia kuimarisha mifumo yake ya ulinzi wa anga, ingawa hakuna ahadi rasmi iliyotolewa hadi sasa.

    Kwa upande wake, Netanyahu aliwasili wakati ambapo uhusiano kati ya Marekani na Israel ulikuwa umetetereka kutokana na mitazamo tofauti kuhusu Iran.

    Kabla ya ziara hiyo, ilitarajiwa kuwa Zelensky angemshinikiza Trump kutimiza ahadi aliyotoa katika mkutano wa kilele wa NATO mwezi huu ya kuipa Ukraine kibali cha kutengeneza makombora ya Patriot ya kuzuia mashambulizi ya anga.

    Kwa muda mrefu Ukraine imekuwa ikitaka makombora ya Patriot ya Marekani; Kyiv inasema makombora hayo yanaweza kutumika kuilinda miji ya Ukraine dhidi ya mashambulizi yanayoongezeka ya ndege zisizo na rubani na makombora ya masafa marefu kutoka Urusi kote nchini humo.

    Hata hivyo, mkutano huo uliofanyika kwa faragha ulimalizika bila tangazo lolote thabiti kuhusu msaada wa kijeshi wa Marekani kwa Ukraine.

    Trump aliandika kwenye mtandao wa Truth Social kwamba mkutano huo "ulienda vizuri sana!"

    Katika ujumbe kwenye mtandao wa X, Zelensky alimshukuru rais wa Marekani kwa "kila tunachofanya kwa pamoja kulinda maisha ya raia wa Ukraine".

    Aliongeza kuwa wawili hao walijadili kuhusu vibali vya Patriot na "mawazo kadhaa ambayo yanaweza kusaidia".

    "Tulizungumzia pia masuala ya kidiplomasia," aliandika. "Ni muhimu mchakato wa kidiplomasia ufufue nguvu mpya."

    Katika ujumbe mwingine tofauti, Zelensky amesema alikutana na wawakilishi wa kampuni ya Marekani inayotengeneza zana za kijeshi ya Lockheed Martin ili kujadili "kuendeleza zaidi ushirikiano wao.

    Soma Zaidi:

  4. WAFCON 2026: Nigeria wachapwa na Malawi 3-2

    Fainali za Mataifa ya Afrika kwa wanawake huko Morocco zimezidi kuchangamka.

    Mabingwa watetezi Nigeria maarufu Super Falcons wameangukia pua baada ya kukubali kichapo cha magoli 3-2 mbele ya Malawi.

    Bila kutarajiwa na wengi, mabingwa hao mara 10 wa Afrika walijikuta wapo nyuma kwa magoli 2-0 yaliyopishana kwa dakika 6 tu mpira ukielekea ukingoni.

    Dakika za mwisho zilishuhudia magoli matatu na kuibua shangwe kwa Malawi ambayo magoli yake matatu yalitiwa kimiani na Temwa Chawinga, huku ya Nigeria yakifungwa na Uchenna Kanu na Rasheedat Ajibade.

    Katika mchezo wa mapema, Zambia waliwafundisha kandanda Misri kwa kichapo cha magoli 6-0 huku Barbra Banda akitia nyavuni magoli matatu.

    Hii leo kuna michezo miwili ya Kundi D: Ghana itakabiliana na Cape Verde, kabla ya Cameroon kupambana na Mali.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Waliofariki kwa tetemeko la ardhi Japan wafikia 13

    Waziri Mkuu wa Japan, Sanae Takaichi, amesema kuwa watu wasiopungua kumi na tatu sasa wamethibitishwa kufariki dunia kufuatia tetemeko kubwa la ardhi lililotokea Jumanne katika kisiwa cha Kyushu, kusini mwa Japan.

    Bi. Takaichi amesema watu wengi bado wanahesabika kuwa hawajulikani walipo au wanasubiri kuokolewa, huku akieleza kuwa vikosi vya uokoaji vinapambana ili kuokoa manusura.

    Operesheni za uokoaji zinaendelea katika duka moja kubwa nchini Japan la Aeon Mall, ambako watu watatu wamethibitishwa kufariki dunia.

    Awali, idara ya zimamoto ya eneo hilo ilisema watu kadhaa walikuwa wamenaswa ndani ya duka hilo huku pia kukiwa na taarifa za matetemeko madogo.

    Eneo la Kumamoto, ambako duka kubwa Aeon Mall liko ni mji ulioko katika kisiwa cha Kyushu, kimoja kati ya visiwa vinne vikuu nchini Japan. Kisiwa hicho cha kusini ni cha tatu kwa ukubwa na cha pili kwa idadi ya watu nchini Japan.

    Afisa wa Mawasiliano ya Umma wa Mkoa huo Akino Sonoda, amesema watu wanane wameokolewa kutoka katika kituo hicho cha Aeon Mall.

  6. Iran na Marekani zashambuliana tena, utulivu wa muda mfupi wasambaratika

    Iran imefyatua makombora kadhaa ya masafa marefu kuelekea vikosi vya Marekani vilivyoko Mashariki ya Kati, katika kile ambacho jeshi la Marekani limesema kilikuwa jaribio la kushtukiza.

    Tukio hilo limekatiza kipindi kifupi cha utulivu kilichokuwa kimeanza kurejesha matumaini ya mazungumzo kati ya pande hizo mbili.

    Kwa mujibu wa Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani (CENTCOM), mashambulizi hayo yalitokea Jumanne saa 5:45 jioni kwa saa za Mashariki mwa Marekani (21:45 GMT). Jeshi hilo linasema makombora yote yalidunguliwa kabla ya kufika maeneo yaliyolengwa, ingawa halikutaja yenyewe.

    Wakati huohuo, Marekani kwa kushirikiana na Saudi Arabia ilifanya mashambulizi dhidi ya maeneo yaliyodaiwa kutumiwa na makundi yanayoungwa mkono na Iran nchini Iraq.

    CENTCOM imesema hatua hiyo ilikuwa ni kulipiza kisasi mashambulizi ya ndege zisizo na rubani yaliyofanywa dhidi ya maeneo ya Marekani katika kipindi cha saa 72 zilizopita.

    Hadi sasa, Iran haijatoa tamko rasmi kuhusu madai hayo.

    Mapigano haya yanahitimisha kipindi kifupi cha utulivu ambacho kilitarajiwa kutoa fursa kwa juhudi za kidiplomasia na mazungumzo kati ya Marekani na Iran.

    Soma Zaidi:

  7. Hujambo Msomaji wetu. Karibu katika matangazo yetu mubashara tarehe ni 29/07/2026.